Sunday, October 13, 2013

Uzee siyo miaka

Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
1
Tokea  nimeamka, Mwenzenu nasononeka.
Jikoni kutosomeka, Heshima inatoweka.

Mtaa unanicheka, Kiangazi na masika.
Nyumbani wananicheka, Naonekana kibweka.
Nafunua nafunika, Hakuna ninachoshika.
Jioni inapofika, Matusi yanigubika.
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
2
Nimeupiga mweleka, Fedha ninazikumbuka.
Niliringa na kucheka, Na kula bila kupika.
Machafu niliropoka, Dunia ikanichoka.
Ujanani nimedeka, Uzeeni sijafika.
Kwa ujinga nasifika, Welevu wananicheka.
Nijuacho  ni kusuka, Kwa marashi mi nanuka.
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
3
Ukweli kutoutaka, Ni bora yangu hulka.
Uongo vema nashika, Ujinga mimi kiraka.
Kesi mbali ninaruka, Hakimu hutonishika.
Kwa jirani naitika,Kwa Mzazi ninafoka.
Marafiki nawasaka, Ndugu shida nawatwika.
Wapambe walinishika,Familia nalitoroka.
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
4
Mengi ya kufikirika, Hakuna kukamilika.
Porojo zangu sifika, Vijiweni zatukuka.
Kitambi chanifumuka, Unyonyaji na kupoka.
Chozi latiririka, Ukweli nikikumbuka.
Ki hali nimenyauka, Ki mali nimekauka.
Hamsini sijavuka, Mkongojo nimeshika
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
5
Najua  utanicheka, Fikira zikipofuka.
Zamani hutokumbuka, Mbeleni katu kufika
Dunia imewehuka, Shetani kishatuteka.
Jembe lako ndugu shika,kiangazi na masika.
Familia yako shika, Na nyumbani nanga weka.
Muda umekwishafika,Akili mbele kuweka
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
6
Wanao ndugu kumbuka, Wasije ukawanuka.
Dunia akawateka, Jirani ulomcheka.
Asili yako kumbuka, Kubali umeumbuka.
Tambua umeanguka, Bora hukuvunjika.
Dira sasa ndugu shika, Dini Muhimu Kufika
Muda huwezi ushika, komaa na chakarika.
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka

7
Ujana ukikufika,Uzee Umekushika.
Ukikwepa  kutukuka,Uborani utafuka.
Waovu watakuruka, Wajinga kutokukuta.
Utoto ukiuruka,Uzee hujauvuka.
Hutajua pa kushika,Furahani hutofika
Mwilini utajanuka, Rohoni hutofufuka
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka
8
Uzee siyo miaka, Ujana sifa epuka.
Balehe ukiivuka, Majukumu ndugu shika.
Yako muhimu kumbuka, Acha zako patashika
Ninamuomba Rabuka, Mkono wangu kushika.
Wazazi wameondoka, Radhi zao sikutaka
Wanikana Tanganyika,  Wa Zenji nimewatoka
Uzee bado Kufika, Ujana unanicheka

Related Posts:

  •  MPAJU WEEK 2020(Disemba 15-22)Uwanja wa Magereza Chuo-Ruanda Mbeyanani kufungua Dimba timu za wasichana?MPAJU FCVS SUPER EAGLES Mpaju FCSUPER EAGLE… Read More
  • LIGI YA MPIRA WA MIGUU KWA WANAWAKE- MKOA WA MBEYAMPAJU FC (a.k.a ATINISU) WAANZA KWA KUKUBALI KIPIGO CHA MAGOLI 9 KWA 1 Tarehe 01 Machi 2021 kulifanyika tukio la kihistoria kwa wanasoka wa Mkoa wa Mbeya. Ligi ya Mkoa kwa Mpira wa Miguu wa Wanawake ilianza ras… Read More
  • Ziara ya Mpaju SC Shule ya Msingi Mpolo 2020 haitasahaulikaKwa mara nyingine, Siku ya Jumamosi tarehe 29 Agosti 2020, Mpaju SC walitembelea shule ya Msingi Mpolo iliyopo Mbalali na kufanya michezo kadhaa ya kirafiki. Hii shule yenye hazina kubwa sana ya Michezo ya nchi hii. Mpaju ime… Read More
  •  MPAJU WEEK 2020“JAMII YETU-KIOO CHETU” Kauli mbiu ya Mpaju Week 2020 ni JAMII YETU NDIO KIOO CHETU. Mpaju SC inaamini changamoto zinazoizunguka jamii yetu zinatokana na kushindwa KWETU kuzitatua. Mpaju SC inaikifikishi… Read More
  • Mpaju Week 2020-YAWA CHACHU KWA SOKA LA WANAWAKE MBEYAMpaju Week 2020 yaleta matumaini ya SOKA LA WANAWAKE MBEYA: Tamasha hili lenye KAULI MBIU YA JAMII YETU NDIO KIOO CHETU, lilifikia tamati siku ya Jumanne tarehe 22 Disemba 2020 pale Uwanja wa Chuo cha Magereza Mbeya, kuwakari… Read More

0 comments:

Post a Comment