Wednesday, April 2, 2014

Mnyonge nyi mnyongeni,Na Haki yake Mpeni



1
Tumlaani shetani, Ubinafsi Shetani.
Hana mpango shambani, Maisha yake angani.
Akishuka aridhini, Atashinda tu majini

Maumivu kijijini,Mijini yahusu nini.
Swali la kutoka lini, Tajiri ajibu nini.
Tajiri afanye nini, Kitufae masikini.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni
2
Mkulima masikini, Uchumi wako ni nini?
Kushinda kwako shambani, Faida yake ni nini?
Jasho lako la shambani, Hasa laliwa na nani?
Maisha kwako ni nini, Useme u kivulini?
Unajipinda shambani, Wanakupunja sokoni.
Kilimo kwanza ni nini, Maumivu kilimoni?
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni
3
Jadala kuu bungeni, Si kilimo ni madini.
Pembejeo si shambani, Zinaliwa tu mijini.
Ujanja sasa nchini,Siasani si shambani.
Mababu wawe shambani, Vijana jaa mijini.
Somo kilimo shuleni, Wanafunzi huwaoni.
Misaada kilimoni,Yaishia tafitini.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni
4

Wakulima vijijini, Hebu jamani semeni.
Mafao yao shambani, Mipango yafanya mboni.
Kodi zote ni shambani, Hadi simu mikononi.
Kuenda uraisini,Kura upate shambani.
Chakula kote nchini, Kinatoka Vijijini.
Wengi wetu wa mijini, Hasa kwetu vijijini.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni
5
Shambani ni vijijini, Mijini pia shambani
Ni wapi leo mjini, Hapakuwa kijijini?
Ufukara mashambani, Umasikini mijini
Waziri awe shambani, Ubunge si luningani.
Reli kufika shambani, Nchi iko duniani.
Waziri daladalani, Mboni yetu ya mijini.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni
6
Kilimo kikumbukeni, Mnyonge msitirini.
Jasho lao masikini, Wabungeni lioneni.
Wasomi wetu vyuoni, Mkulima mjueni.
Wataalamu nchini, Faida yenu ni nini?
Sayansi yetu jamani, Itufaacho ni nini?
Tuache ulimbukeni, Tujali kwetu nyumbani.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni

7


Elimu ziko mijini, Shambani abaki nani.
Shamba si usanii, Mkulima ale nini?
Wajanja si vijijini, Nakana huo Utani.
Wajinga wengi mijini, Tukibisha tubisheni.
Loliondo kumbukeni, Babu naye wa mjini?
Tamaduni tuthamini, Taaluma   zi shambani.
Mnyonge tumnyongeni,La Hakiye tumpeni





Related Posts:

  •  MPAJU WEEK 2020(Disemba 15-22)Uwanja wa Magereza Chuo-Ruanda Mbeyanani kufungua Dimba timu za wasichana?MPAJU FCVS SUPER EAGLES Mpaju FCSUPER EAGLE… Read More
  • LIGI YA MPIRA WA MIGUU KWA WANAWAKE- MKOA WA MBEYAMPAJU FC (a.k.a ATINISU) WAANZA KWA KUKUBALI KIPIGO CHA MAGOLI 9 KWA 1 Tarehe 01 Machi 2021 kulifanyika tukio la kihistoria kwa wanasoka wa Mkoa wa Mbeya. Ligi ya Mkoa kwa Mpira wa Miguu wa Wanawake ilianza ras… Read More
  •  MPAJU WEEK 2020“JAMII YETU-KIOO CHETU” Kauli mbiu ya Mpaju Week 2020 ni JAMII YETU NDIO KIOO CHETU. Mpaju SC inaamini changamoto zinazoizunguka jamii yetu zinatokana na kushindwa KWETU kuzitatua. Mpaju SC inaikifikishi… Read More
  • Mpaju Week 2020-YAWA CHACHU KWA SOKA LA WANAWAKE MBEYAMpaju Week 2020 yaleta matumaini ya SOKA LA WANAWAKE MBEYA: Tamasha hili lenye KAULI MBIU YA JAMII YETU NDIO KIOO CHETU, lilifikia tamati siku ya Jumanne tarehe 22 Disemba 2020 pale Uwanja wa Chuo cha Magereza Mbeya, kuwakari… Read More
  • Ziara ya Mpaju SC Shule ya Msingi Mpolo 2020 haitasahaulikaKwa mara nyingine, Siku ya Jumamosi tarehe 29 Agosti 2020, Mpaju SC walitembelea shule ya Msingi Mpolo iliyopo Mbalali na kufanya michezo kadhaa ya kirafiki. Hii shule yenye hazina kubwa sana ya Michezo ya nchi hii. Mpaju ime… Read More

0 comments:

Post a Comment