Sunday, May 17, 2020

Udhibiti wa Idadi ya Wachezaji wa Kigeni Ligi Kuu Tanzania Bara

Maamuzi ni vema Yakazingatia vizuri WAKATI WETU.

Kama nimeelewa hoja, ni kuwa kwa kuwapunguza wachezaji wa kigeni walau kwa asilimia walau 50, kuna uwezekano tukaongeza nafasi ya wachezaji wa nyumbani kupata nafasi katika timu zao za kwanza za vilabu vyetu. Na kimsingi kwa kama hilo litatokea kuwa hivyo matarajio ni kuwa

1.       Wachezaji watapata kucheza mechi nyingi na zenye ushidani za kutosha kuongeza uimara wa kuweza kutupatia matokeo mazuri zaidi katika timu yetu ya taifa.

2.       Vilabu vya Tanzania kuthamini wachezaji wa umri mdogo AMBAO NI WAZAWA na ikiwezekana kuwaandaa wenyewe kupitia timu zao za watoto wadogo kama sio kuziimarisha kabisa hizo timu.

Hili linaweza kuwa sahihi, KWA UPANDE FULANI. Yaani, ukichukulia kuwa timu kama Simba, Azam au Yanga, zina mchango mkubwa katika timu ya Taifa, kwa kutoa wachezaji wengi na pengine kwa maendeleo ya mpira nchini. Pamoja na kuwa na timu za vijana,bado mara nyingi  kipaumbele ni mafanikio yao katika mashindano makubwa, na hivyo uhitaji wa wachezaji wenye uzoefu na uwezo mkubwa ni chaguo lao zaidi ya wachezaji wachanga.Kwa hiyo, Moja ya sababu ya kupenda kusajili wachezaji wa kigeni, ambao wanaamini na kwa hivi karibuni wamekuwa wakisaidia kufanya vizuri kwa timu hizo, inaweza kuwa ni TAHADHARI YA KUPATA HASARA YA KIPESA kwa kutumia pesa nyingi kuandaa hao vijana wakati nafasi ya hao vijana kufanya vema kwa haraka kwenye mashindano makubwa ni ndogo. Kwa hiyo inakuwa ni hasara kwao.

Kama hoja ni hiyo, naamini pia mtazamo unachukulia kuwa:

1.       Timu nyingi za Ligi Kuu, hasa zile zenye mchango mkubwa wa wachezaji katika timu ya TAIFA, zinatumia wachezaji wa nje kwa kiwango kikubwa katika mechi zao za ligi na zina uwezo wa kuchukua wachezaji walau hadi 10, kama sheria inavyowataka kwa sasa.

2.       Idadi inayopunguzwa ya wachezaji wa kigeni, haitapelekea kuharibika kwa mafanikio ya kibiashara ya timu na kusababisha timu hizo kushindwa kwenda kwenye hatua kubwa za mashindano amabzo ndio muhimu kwa ubora wa wachezaji wa nyumbani

3.       Mazingira mengine ya uendeshaji wa mpira kama vile timu za watoto wadogo na malipo ya wachezaji wa aina zote ni mazuri kwa kila timu.

4.       Na pengine, mchezo wa mpira wa miguu kwetu umefikia hatua nzuri ya Kitaalamu. Hivyo wachezaji wakipewa nafasi watatumikia vema na waajiri au vilabu viko tayari kulipa stahiki zao bila shida.

Kuna watu wanaamini kuwa hii sio njia sahihi, ukisoma maandiko katika mitandao, watu kadhaa kutoka Tanzania, akiwemo Haji Manara (Mkuu wa Idara Ya Habari Na Mawasiliano ya Klabu Bingwa Tanzania Bara na mabingwa wa kihistoria kwa mechi za kimataifa nchini Tanzania, mtoto wa mmoja wa mastaa wakubwa katika historia ya mpira wa miguu nchini Tanzania, Haji Sunday Manara-http://www.dar24.com/haji-manara-apinga-kupunguza-wachezaji-wa-kigeni/). Kwao njia sahihi ingekuwa kuboresha VITUO VYA WATOTO wadogo na kuweza kuandaa vipaji vyetu ili vijana waweze KUIVA KITAALAMU katika mchezo huu. Kwao, pengine kupunguza wachezaji hukuondoi mzizi wa tatizo, kwa sababu  hata idadi ya wachezaji wa nje sio kubwa kiasi cha kusema kinaathiri ubora wa timu ya taifa. Na pengine kufanya hivyo kutapunguza zaidi nafasi ya timu kubwa chache zenye wachezaji hao wa kigeni wengi, za nchini kuweza kushindana kimataifa na hivyo kushusha mafanikio yao kibiashara pia. 

Ukisoma   https://ghanasoccernet.com/egyptian-fa-to-reduce-foreign-players-quota, unaweza kuona jinsi swala hili linavyochukuliwa na mashabiki wa soka baada ya Misri kupunguza idadi kutoka wachezaji watano mpaka wanne wa kigeni.

Ulaya pia swala linaloendana na hili limewahi jadiliwa mara kadhaa. Ukisoma kwenye maandiko kama lile la (Smokvina, 2013) kuhusu taratibu za idadi za wachezaji wenyeji na wageni, na hata wale walio chini ya miaka 21, bado inaonekana lengo hasa la taratibu za namna hii, ni kujaribu kuweka usawa kati ya biashara za timu husika na manufaa ya nchi. Japo kuna hoja kadhaa za kuashiria kuwa matokeo ya mipango hii bado haijatoa mafanikio ya kuridhisha kuweza kusema ni taratibu sahihi kwa malengo yake. Wengine wanaamini ni mifumo wenye mapungufu ya kisheria pia. Yaani, uhuru wa wachezaji kutoka kutoka nchi moja hadi nyingine ni kama unaingiliwa pia kwa kiasi fulani.

Changamoto kubwa ninazoiona ni kupata uwiano sahihi wa maslahi. Wote tunataka mafanikio ya nchi katika soka, lakini tofauti ni njia gani ni sahihi kuyafikia mafanikio hayo. Mimi kama shabiki, ninachotaka ni furaha ya kila siku mpaka nakufa. Kama mteja namba moja ninachohitaji ni kuona timu yangu ni bora kuliko zote ulimwenguni. Na upande mwingine, kama mzalendo na mwenye kuhitaji maendeleo ya kitaifa, napenda kuona mtanzania anapewa kipaumbele kwanza, ili pesa yangu ijenge nchi yangu pia. Swala la kuandaa vijana au wachezaji wa taifa, nitapenda lifanyike lakini lisizuie uwezo wetu wa kimataifa kila mwaka. 

Binafsi naamini Simba, Yanga na zinginezo ni timu saidizi tu za serikali katika kuandaa timu ya taifa au kuendeleza mchezo huu nchini.Serikali ina jukumu la kuweka mazingira mazuri kwa wote ikiwemo timu kubwa katika kuhakikisha ndoto za timu, mashabiki,wananchi na vijana machipukizi zinatimia. Baadhi ya raia Afrika ya Kusini, waliwafukuza watanzania na watu wa mataifa mengine wakiamini ndio chanzo cha wao kukosa kazi na pengine maisha mazuri.Wanaweza kuwa sahihi, lakini siamini kama huo ulikuwa mzizi wa maisha yao kuwa magumu au kuwa hakukuwa na namna nyingine ya kulizuia hilo. Kupunguza maumivu ya kichwa unapougua malaria ni jambo jema ili walau uweze kuendelea kuandika porojo muhimu kama hizi, lakini kuondoa wadudu wa malaria hata kama ni kwa sindano, ni muhimu sana ili kudumu katika hali nzuri kiafya dhidi ya malaria. Serikali isisite kuanza safari ya kuondoa wadudu wa malaria kwa sababu hakuna mwingine wa kusaidia katika hilo.

Kwenye michezo, wimbo wa tuwajali vijana na vijana taifa la kesho nimeusikia miaka Zaidi ya thelathini sasa. Sio kwamba hakuna kinachofanyika, la hasha, ila siamini kama kinachofanyika kinatosha. Pengine tunasubiri MUDA utulazimishe. Kuna wengi wanafanya mengi mazuri, kwa jitihada binafsi hapa nchini naamini.Ila siamini kama inatosha kwa mtu au taasisi binafsi kufanya jambo la kitaifa bila nia na msaada madhubuti wa kimiundombinu kutoka serikalini. Namkumbuka mwalimu wangu Mdachi Kombo, aliyekuwa mchezaji wa timu ya Majimaji. Alifanya kazi kubwa sana pale Songea, kwa kuanzisha timu ya vijana wadogo, nikiwemo mimi na mashindano ya timu za vijana na hadi viongozi wa Majimaji wakaburudika sana. Vijana kama Masumbuko Makalisha na Amani Simba, walifanya vema Mtibwa na Simba,kwa kiasi kikubwa maandalizi hayo yaliwasaidia. Swali ni wapi alipo Mdachi Kombo? Nini kilimkuta akaacha kuzalisha wachezaji wengine? Na cha ajabu hao wachezaji wawili sijui ni yupi aliwahi kuchezea Majimaji. Alichofanya Mdachi Kombo ni kitu cha kujitolea, ambacho kimsingi atalipwa na MUNGU. Kimsingi kitu kama hiki kilipaswa kupewa mazingira mazuri kumsaidia Mdachi Kombo ama kufanywa na serikali ili kiwe cha kudumu.

Serikali inapaswa kujitolea Zaidi kwenye hili kuliko taasisi au mtu mwingine.Wakati Napata habari kuwa Gharib Said Mohammed (GSM), anayehusishwa na Dar Young African, mabingwa wa kihistoria wa kombe la Tanzania Bara, kuwa ni kati ya wachezaji watimu ya watoto ya Liverpool ya Mdachi Kombo pale Songea, nilifurahia sana mafanikio yake kifedha, ila nikaahidi kuwa nikipata nafasi ya kuongea naye, nitamuuliza kwa nini hakuanzisha timu za vijana kama ambavyo Mdachi Kombo alivyofanya.Nadhani Mo Dewji, mdhamini wa timu niipendayo pia, aliliweka hili wazi kuwa anahangaika na Simba kwa sababu kibiashara JINA la Simba linaweza kumpa uwiano mzuri wa Maslahi kuliko kuanza chini.

Najivunia sana kuwa mmoja wa wanaMpaju FC (https://www.mpajusc.com/), naamini mzee Mdachi Kombo,atajivunia pia kuona kijana wake angalau kafuata nyayo zake. Kama ningepewa nafasi ya kushauri, nadhani ningesema yafuatayo:-

1.       Timu yenye uwezo wa kusajili hata wachezaji Thelathini wa KIGENI, ipewe uhuru wa kufanya hivyo. Muhimu ni kuangalia ni jinsi gani, taifa linaweza kupata thamani nzuri kutokana na uwepo wa hao wachezaji. Leo hii akiwepo Messi katika timu zetu nchini, radha ya mpira na hata biashara yake itapanda na kuleta mambo mengi chanya katika nchi. Labda waingereza wao utaratibu huu unaweza usiwafae kutokana na hatua waliyopo kimaendeleo. Lakini hata sisi huenda tukifika hatua nyingine tutabadili muundo ili kwendana na wakati, ila kwa sasa nadhani tunahitaji zaidi kuufanya mchezo uwe Elimu, Burudani, Biashara,Ajira,Afya,Malezi na Furaha nchini, zaidi ya kufanya vizuri kimataifa kama taifa. Acha Simba na Yanga ziende na zifike popote zinapoweza kama timu.

2.       Jukumu la mafanikio ya timu ya Taifa na vijana wenye vipaji ni jukumu la serikali. Hivyo serikali, iweke na kusimamia sheria ya ligi za watoto. Hakuna sababu timu zote kupenda kuwa madaraja ya juu badala ya kupenda mpira na mafanikio yake katika ngazi zote. Fikiria kama kila Kila kata au Wilaya iwe na ligi kama ya Mpaju Cup http://mpaju.blogspot.com/2019/09/mpaju-cup-2019-yahitimishwa-na-kiongozi.html. Ligi kama hii inahitaji pesa kidogo tu kuianzisha na baadae itajiendeleza yenyewe baada ya wazazi kuona na kufahamu kuwa nayo ni sehemu ya elimu na malezi kwa vijana wao.

3.       Sijui kama mashindano ya kitaifa ya shule za sekondari na msingi ni ya muhimu sana kwa wakati tulionao. Naamini tunahitaji taratibu,muda,maeneo na taasisi binafsi nyingi zinazojishughulisha na michezo na sanaa kwa watoto na jamii yetu. Kama tunaweza kupambana na magonjwa, hakuna tunachoshindwa kuweka na kusimamia mikakati ya michezo kwa ajili ya vijana. Tuwe na vituo vya kujifunza muziki,mpira na kadhalika mitaani. Mashuleni watoto wasome vyote kama masomo na viwanja vyao na maeneo yao yatumike kama sehemu za majaribio na mazoezi au mashindano ya kirafiki. Sidhani kama tunahitaji mashindano ya mashuleni na kuwakusanya vijana kwenye umiseta na umishumta kama zamani. Wakati umepita wa kufanya hivyo. Tanzania House Of Talents (THT) iko Dar Es Salaam tu, kwa nini? Viwanja vya JK viko Dar. Kila kitu ni DSM, kwa nini? Uwiano wa maslahi bado ni bora Dar....! Mbeya hata kiwanja Ngoma kimekufa kabisa, mahali ambapo naambiwa wachezaji kama Sekilojo Chambua wanapafahamu pia. 


4.       Tuwafanye watoto kuwa kiini katika dira yetu ya michezo, mengi yatafunguka ya leo na ya kesho. Najua wabeijingi watauliza, kwa nini watoto na sio wao? Jibu la hilo swali kwangu mimi ni sijui. Sijui tumelogwa na nani? Angalia michezo ya vijana, si ajabu kuona mpaka leo watoto mtaani wanacheza bila viatu. Sasa vipi kuhusu sheria za mpira au misingi ya kitaalamu ya michezo wataijuaje?Tuanze leo na tuanze na Mpaju Sports Centre.    

Kocha Ali Mkumbukwa Akiwa na Vijana wa U-12 Mpaju FC wakati wa Mapumziko uwanja wa FFU Mbeya

Mpaju FC wakiwa kwenye Picha ya Pamoja wakati wa Tamasha la Mpaju Week 2019 Uwanja vya Magereza Mbeya


Mpaju FC U-12 wakisubiri Kuchuana na Shule Msingi Mpolo Wasichana U-15 Uwanja wa Magereza Mbeya wakati wa Mpaju Week 2019


0 comments:

Post a Comment